Saturday, October 6, 2012

WANAFUNZI 138 WA KIDATO CHA NNE WAKATISHA MASOMO

WANAFUNZI 138 wa kidato cha nne katika shule ya sekondari Senga wilayani Geita,wamekatisha masomo yao kutokana na mwamko mdogo wa elimu na kipato duni kinachowakabili wazazi na walezi wao.

Mkuu wa shule hiyo,Mwalimu Magoma Komesi,amesema hayo kwenye mahafari ya tano ya kidato cha nne yaliyofanyika juzi wakati akisoma taarifa ya shule hiyo kwa mgeni rasim meneja wa Benki ya NMB wilaya ya Geita Bw.Mdasi Kalema.

Mwalimu Komesi amesema kuwa kati ya wanafunzi 241 kati yao wavulana 177 na wasichana 64 waliosajiliwa kujiunga na masomo shuleni hapo mwaka 2009 ni wanafunzi 103 kati yao wavulana 85 na wasichana 18 ndiyo wamefanikiwa kufika kidato cha nne na kusajiliwa kufanya mtihani wa Taifa mwaka huu.

Amesema tatizo hilo linatokana na wazazi na walezi kuishi kwa kutegemea kilimo na uvuvi ambapo kutokana na hali ya hewa kubadilika na kujitokeza ukame wazazi hukosa mazao ya kuuza ili kuwaendeleza watoto wao,ambao kutoka na hali hiyo baadhi yao wameamua kuoa na kuolewa.

Hata hivyo katika risala ya wahitimu hao iliyosomwa na mwanafunzi Waziri Sabaganga wamesema shule hiyo inakabiliwa na upungufu wa walimu ,vyumba vya madarasa na maabara hali ambayo imekuwa ikiwasababishia kutofanya vizuri katika mitihani yao na hivyo kuiomba serikali kuweka mikakati madhubuti ya kuondoa tatizo hilo.

Kwa upande wake mgeni Rasmi katika mahafari hao meneja wa NMB Geita Bw.Kalema amewataka wanafunzi hao kujiepusha na vitendo viovu kama matumizi ya dawa za kulevya na ngono  ambavyo vinaweza kukatisha ndoto zao kuendelea na elimu ya juu kwa manufaa ya familia zao na Taifa kwa ujumla.
                                                    MWISHO

No comments:

Post a Comment