Wednesday, October 3, 2012

ASKARI NA KASHFA NZITO

Na Magreth Chaba,Chato.

ASKARI wa kituo kidogo cha Polisi cha Buziku wilayani Chato mkoani Geita wamekumbwa na kashfa kubwa baada ya kutuhumiwa kuwakamata na kuwatesa wananchi wawili waliokuwa wamelala kwenye nyumba ya wageni ya Buziku Hill Guest House hali iliyosababisha mmoja wao kupoteza maisha.

Tukio hilo limetokea Oktoba 3 mwaka huu majira ya saa 5;30 usiku wakati wananchi hao wakiwa wamejifungia ndani ya vyumba vyao wakiendelea kunywa pombe(Bia) ambapo askari polisi walifika eneo hilo na kuwaamuru kufungua milango yao kwa lengo la kuwafanyia upekuzi.

Baada ya wananchi hao kukaidi amri ya polisi,askari hao walilazimika kutumia nguvu na kufanikiwa kuvunja milango ya vyumba hivyo kisha kuanza kuwaadhibu watu hao kabla ya kuwapeleka kwenye kituo kidogo cha polisi kilichopo kwenye kata hiyo.

Aidha ameelezwa kuwa baada ya kipigo kikali vijana hao walipelekwa kwenye kituo hicho cha polisi na kabla ya kuhojiwa hali zao kiafya zilibadilika ghafra na kulazimika kuwakimbiza kwenye Kituo cha afya cha Bwanga kwaajili ya matibabu lakini kutokana na kuonekana mahututi zaidi walikimbizwa hospitali ya wilaya ya chato.

Kaimu kamanda wa Polisi mkoa wa Geita Paulo Kasabago amekiri kuwepo kwa tukio hilo na kudai kuwa askari wake walifika eneo la tukio baada ya kuelezwa na raia mwema kuwa kuna watu wanaosadikiwa ni majambazi kutokana na mazungumzo waliyokuwa nayo wakati wakinywa pombe nje ya guest hiyo kabla ya kuingia ndan ya vyumba vyao kulala.

Ameeleza kuwa baada ya askari wake kuingia ndani kwa lengo la kuwakamata watuhumiwa na kuwafanyia upekuzi,mmoja wa watuhumiwa hao alimkwida koo askari PC Mwidin hali iliyosababisha askari wenzake kutumia nguvu kubwa ili kumsuru mwenzao kujeruhiwa.

Amesema baada ya kufanikiwa kuwatoa ndani ya vyumba vyao na kabla ya kuwafikisha kituoni,kundi kubwa la wananchi waliokuwa wanatoka kutazama soka la ulaya kwenye moja ya ukumbi uliopo kijijini hapo walifika kwenye tukio na kuanza kuwasaidia polisi kuwapeleka watuhumiwa hao lakini kutokana na kukataa kata kata wananchi waianza kuwaadhibu huku mkuu wa kituo hicho cha polisi akilazimika kuwazuia.

Baada ya kumalizika upekuzi wa askari walifanikiwa kukuka kiasi cha shilingi laki 5 ndani ya chumba kimoja na kingine walikuta kiroba cha mfuko uliokuwa na mawe yanayosadikiwa kuwa ni ya dhahabu pamoja na chupa moja ya pombe aina ya Bia.

Kadhalika wakati watuhumiwa hao wakiendela kupata matibabu kwenye hospitali ya wilaya ya chato,mmoja wao alifariki dunia wakati akiendelea kutibiwa.

Kasabago amemtaja aliyepoteza maisha kuwa ni Gilbert Ntabonwa mkazi wa kijiji cha Kakeneno na mzaliwa wa Kibondo mkoani Kigoma huku majeruhi mwingine David Vyamana hali yake ikiendelea vizuri.

Kufuatia hali hiyo jeshi hilo linawashikilia askari wake wanne kwaajili ya uchunguzi kutokana na kutuhumiwa na kuhusika na tukio la kujeruhi na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kwamba uchunguzi utakapo kamilika hatua za kisheria zitachukuliwa.

Amewataja askari wanaoshikiliwa kuwa ni OCS wa kituo hicho Sajent Raulens Bendera,PC Mwidin,PC abdalah na PC Yusuph wote wakiwa ni askari wa kituo kidogo cha Buziku.

Mganga mkuu wa hospitali ya Wilaya ya Chato Dk Pius Buchukundi amekiri mmoja wa majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo kufariki dunia wakati akiendelea na matibabu.

Amesema uchunguzi wa kitabibu ulibaini kuwa marehemu alikuwa amejeruhiwa vibaya kutokana na kipigo hali iliyosababisha damu kuvujia ndani ya mwili na hivyo kupelekea mauti hayo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment